WIZARA YA AFYA YAKAMILISHA MRADI WA HEWA TIBA( OXYGEN) KATIKA HOSPITALI YA RUFAA YA MKOA WA ARUSHA, MOUNT MERU
Wizara ya Afya imetimiza hatua muhimu katika kuboresha huduma za afya kwa kukamilisha mradi wa uzalishaji wa hewa tiba (oxygen) katika hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Arusha, Mount Meru, mradi ambao utaongeza upatikanaji wa hewa hiyo muhimu kwa wagonjwa, kupunguza gharama za upatikanaji wa hewa tiba, na kuimarisha huduma za afya katika hospitali hiyo pamoja na maeneo jirani.
Kaimu Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Mount Meru, Dkt. Kipapi Mlambo, allipokea rasmi hati ya kukamilika kwa mradi huu kutoka kwa wataalamu wa kampuni za NOVAIR kutoka Ufaransa na SIGMA, ambao walikuwa washirika wakuu katika utekelezaji wa mradi huu.
Mtambo huu wa kisasa una uwezo wa kuzalisha mitungi 20 ya hewa tiba (oxygen) ndani ya saa 24, hivyo kutatua changamoto ya upatikanaji wa oxygen hospitalini hapo na kuongeza ufanisi wa vitengo vya dharura kama ICU, Chumba cha upasuaji, na wodi zinazohitaji hewa tiba kwa wingi.
Ufanisi wa mradi huu ni sehemu ya juhudi za Serikali kuboresha huduma za afya na kuongeza uzalishaji wa hewa tiba nchini, ili kuokoa maisha ya watu na kuhakikisha huduma bora kwa wagonjwa.