Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amehitimisha maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma ya mwaka huu, kwa kuhimiza taasisi zote zenye mifumo na zinazobuni mifumo zihakikishe inasomana.
Aidha, amezindua mifumo miwili ya kielektroniki ukiwemo Government Enterprises Service Bus (GovESB), unaowezesha mifumo ya Serikali kuwasiliana na kubadilishana taarifa, pamoja na mfumo wa e-Wekeza unaomuwezesha mtumishi wa umma kuwekeza katika Mfuko wa Faida (Faida Fund).
Akitoa hotuba kwenye viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma, kwa niaba ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, wakati wa kilele cha maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma, ambayo Baraza la Taifa la Ujenzi (NCC) limeshiriki, Waziri Mkuu amesema,
:”Mifumo hiyo inatupunguzia vishawishi na kuondoa mianya ya rushwa. Inawabana wala rushwa, kwa hiyo, watakaoshindwa kujiunga na mfumo wa GovESB hadi Julai 30, mwaka huu, watakuwa ndio wala rushwa na itabidi wajieleze ni kwanini hawajajiunga,”.
Kwa niaba ya Rais, Waziri Mkuu amewapongeza watumishi wa umma nchini na kusema, ametambua ubunifu wao. Maadhimisho hayo yalianza Juni 16, mwaka huu yakiwa na kauli mbiu isemayo Himiza matumizi ya mifumo ya kidijiti kuongeza upatikanaji wa taarifa na kuchagiza uwajibikaji.
NCC imeshiriki na kutembelewa na viongozi mbalimbali akiwemo Naibu Waziri, Ofisi ya Rais-Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deus Sangu, Katibu Mkuu wa UTUMISHI, Bw. Juma Mkomi na Mkurugenzi Benard Makhanda na Naibu Mkurugenzi Jafari Maganga, kutoka ofisi hiyo.